KAMA
si Mungu, maisha yangu si lolote. Sina ujanja wa kufanya chochote bila
msaada wake, hii ndiyo sababu inayonifanya siku zote nimuinue na
kumtukuza kwa nguvu kwa maana yeye ndiye mwongozo wangu.
Karibuni
marafiki zangu katika uwanja wetu ambao hupanua mawazo yetu ndani ya
ulimwengu wa mapenzi. Leo nahitaji kuzungumza nanyi jambo moja muhimu
sana; kujipandisha thamani kwa mpenzi wako.
Kuna wakati inatokea
kwenye uhusiano, mmoja wao (hasa mwanamke) akadhauriwa na mpenzi wake na
kuonekana wa kawaida tu. Athari kubwa zaidi katika kuonekana wa kawaida
au kudharauliwa ni kuachana wakati wowote – kwa ghafla.
Mara nyingi
tendo la kuachana kwa wenzi wa aina hii huwa hakuna sababu kubwa sana.
Jambo dogo tu, linaweza kukatisha uhusiano, lakini kumbe ndani kuna siri
nyingine kubwa zaidi; kushuka thamani kwa mpenzi wako.
Marafiki
zangu, wakati uhusiano unapofikia kwenye hatua hii huwa ni hatari sana
na uamuzi wa kuachana hupewa nafasi kubwa sana tena kwa pande zote.
Habari mbaya zaidi ni kwamba, hata kama wahusika watakuwa wana ndoa,
huwa si kigezo kikubwa sana kwao, badala yake hufikiria kuachana kama
ndiyo kitulizo cha mioyo yao.
HEBU TUJIFUNZE
Nazungumzia kuhusu thamani. Ni
somo linalohitaji utulivu mkubwa wa akili na utayari wa ubongo.
Ninaposema kushuka thamani namaanisha kupungua kwa umuhimu au kupotea
kabisa.
Kubwa ambalo utakuwa umebaki nalo (labda) ni kukutana kwa
ajili ya mapenzi tu. Hawezi kukushirikisha katika mambo yake kwa sababu
huna thamani kwake.
Kwa bahati mbaya ni kwamba, ukishushwa thamani,
mara nyingi unaweza usigundue hilo hivyo kuendelea na maisha kama
kawaida katika mtindo ambao kumbe tayari mwenzako ameshakubadilisha
daraja.
UTAJUAJE KUWA UMESHUSHWA THAMANI?
Ninachohitaji
kuzungumza nanyi marafiki zangu ni namna ya kujipandisha thamani ili
mpenzi wako asikuchoke wala kukushusha au kukuona wa kawaida. Kila
wakati akione wewe ni muhimu na akufanye namba moja katika maisha yake
lakini kabla sijafika hapo nataka kwanza mfahamu dalili atakazozionyesha
mwenzako kuonesha kwamba ameshakushusha thamani.
(i) Mawasiliano hupungua
Hapa
inategemea na kasi ya mawasiliano mliyokuwa nayo mwanzoni lakini kwa
kiwango chochote kile huanza kupungua. Kama alikuwa na kawaida ya
kuwasiliana nawe mara kwa mara akikueleza mambo mbalimbali – hata madogo
tu, kuhusu mwenendo wa siku yake, ataacha.
(ii) Msiri kupitiliza
Kulingana
na kiwango cha uhusiano wenu, ataanza kuwa msiri kwa baadhi ya mambo
yake. Hata kama anafanya jambo fulani zuri kwa ajili ya maisha yenu ya
baadaye, hatakuambia. Unaweza kushtukia tu kusikia kwa watu kuwa
mwenzako ameagiza gari au amenunua kiwanja mahali na pengine ameshaanza
ujenzi bila kukujulisha.
(iii) Hukupuuza
Kama awali alikuwa na
kawaida ya kukusikiliza, sasa ataanza kukupuuza. Unaweza kumwambia jambo
lenye manufaa makubwa sana kwenu lakini asilichukulie umakini. Hii ni
dalili kwamba wewe huna thamani kwake.
(iv) Hataki maswali
Mara
nyingi mtu wa aina hii huwa na tabia ya kutokutaka kujadiliana kwa hoja.
Kwa mfano hataki kuulizwa alipokuwa na ratiba zake zijazo. Huanza kuwa
na jazba na hataki kabisa maswali yoyote kuhusu utaratibu wa maisha
yake.
Ukiona alama hii ujue kuwa tayari mwenzako ameshakushusha
thamani. Marafiki, natamani kuendelea zaidi lakini nafasi yangu ni
ndogo. Kwa leo naomba kuweka kituo kikubwa hapa, wiki ijayo tutaendelea,
USIKOSE!
Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi anayendikia
Magazeti ya Global Publishers, ameandika Vitabu vya True Love, Let’s
Talk About Love na All About Love vilivyopo mitaani.
No comments:
Post a Comment